Showing posts with label siasa. Show all posts
Showing posts with label siasa. Show all posts

Monday 2 March 2015

VIONGOZI WAONGOZA KUMUAGA MAREHEMU KOMBA KARIMJEE

Rais Kikwete (katikati) akiwa na makamu wake Gharib Bilal (kushoto) na Anna Makinda katika viwanja vya Karimjee ili kumuaga marehemu Kapteni John Komba.
Rais Mstaafu Benjamin Mkapa (wa pili kulia) akiwa na mkewe Anna (wa tatu kulia) wakiwasili viwanja vya Karimjee.
Waziri mkuu aliyejiuzulu,Edward Lowassa (kulia)akisalimiana na Mkapa.
Spika wa Bunge, Anna Mkapa (kushoto) akiwa na Mkapa.
Mbunge wa Kinondoni Idd Azzan (kushoto) akiwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe.
Aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba (kulia) akiwa viwanja vya Karimjee.
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba (kulia)akisalimiana na mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombale.
Wake wa marehemu Komba, katikati ni mke mkubwa, Salome, na kulia ni mke mdogo.
Miongoni mwa wanafamilia wa marehemu Komba.
Mwili wa marehemu John Komba ukiingia Karimjee ili kuagwa na wananchi na viongozi mbalimbali leo jijini Dar.
+

Tuesday 30 December 2014

MAMA LWAKATARE HAFIKIRII KUGOMBEA UBUNGE MWAKANI



Mbunge wa Viti Maalum CCM ambaye pia ni Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Mikocheni B Assemblies of God jijini Dar, Dk. Getrude Rwakatare (pichani) ameibuka na kusema hafikirii kugombea nafasi hiyo mwakani.Mbunge wa Viti Maalum CCM ambaye pia ni Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Mikocheni B Assemblies of God jijini Dar, Dk. Getrude Rwakatare.
Akizungumza na gazeti hili juzi jijini Dar, Mama Rwakatare alisema amebaini kwenye siasa kuna watu wanataka kutumia nafasi hiyo kumchafua jambo ambalo linampa wakati mgumu ikizingatiwa kuwa ana watu wanaomwamini kiroho.
“Sifikirii kwa sasa kugombea ubunge mwakani, siasa ina mambo mengi sana, bora niendelee kumtumikia Mungu, kama wazo litanijia tena ni hapo baadaye,” alisema Mama Rwakatare.Mama Rwakatare ambaye pia ni mmiliki wa Shule za St. Mary’s alisema anaamini katika kumtumikia Mungu zaidi kuliko kujikita kwenye siasa.
Shule za St Mary’s zinazomilikiwa na Mchungaji Rwakatare zimekuwa juu kielimu karibu kila kona ya nchi.
Kwa mfano, Shule ya Sekondari ya St. Mary’s International iliyopo Mang’ula, Ifakara, Morogoro imekuwa ya kwanza kiwilaya, St. Mary’s International Kihonda Morogoro Mjini imekuwa ya pili kiwilaya na ya tano kimkoa na imetoa mwanafunzi bora Afrika Mashariki wa kwanza katika mashindano ya insha.
Bado shule za St. Mary’s ziliendelea kufanya vizuri kwani St. Mary’s Tabata jijini Dar ilikuwa ya sita kiwilaya na wanafunzi wote walichaguliwa kuendelea kidato cha tano.
Shule ya St. Mary’s Mbagala ilishika nafasi ya tano kiwilaya na wanafunzi wote wa darasa la saba walichaguliwa. Shule ya St. Mary’s Mbeya ilikuwa ya pili kiwilaya na ya sita kimkoa, mwaka jana ya kwanza kiwilaya na ya tatu kimkoa, watoto wote walichaguliwa.
Mkurugenzi wa shule hizo, Mama Rwakatare alisema shule zake zinafanya vizuri kutokana na kuwa na walimu wenye sifa.“Walimu wote wana sifa, ndiyo kigezo tunachosimamia ili kuajiri. Hii imetusaidia sana shule za St. Mary’s kuwa bora,” alisema mama Rwakatare.
+

Monday 29 December 2014

NYALANDU ATANGAZA RASMI NIA YA KUWANIA URAIS 2015

 Waziri wa Maliasili na Utalii, Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazalo Nyalandu alisalimia wananachi baada ya kuwasili na mkewe Faraja Kota kwenye Mkutano wa jimbo uliofanyika jana kwenye Uwanja wa Michezo wa Ilongelo, jimboni humo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazalo Nyalandu alisalimia wananachi baada ya kuwasili na mkewe Faraja Kota kwenye Mkutano wa jimbo uliofanyika jana kwenye Uwanja wa Michezo wa Ilongelo, jimboni humo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazalo Nyalandu alisalimia wananachi baada ya kuwasili na mkewe Faraja Kota kwenye Mkutano wa jimbo uliofanyika kwenye Uwanja wa Michezo wa Ilongelo, jimboni humo.
 Mwimbaji wa muziki wa Injili, Frola Nkone akiimba kutumbuiza wakati wa mkutano huo.
Mwanamuziki wa muizki wa Injili, Rose Mhando akiimba kutumbuiza wananchi katika mkutano huo wa Nyalandu.
Wasanii wa kikundi cha Makomandoo cha mjini Singida wakitumuiza wakati wa mkutano huo.
Wadau wakifurahia burudani wakati wa mkutano huo wa Nyalandu.
Steve Nyerere ambaye ni Msanii na Kamanda wa Umoja wa Vijana wa CCM, akizungumza kabla ya kumwaga vimbwanga vyake vya kuingiza sauti za viongozi mbalimbali wakati wa mkutano huo wa Nyalandu.
KABLA YA MKUTANO
Nyalandu na Mkewe Faraja Kota wakiingia kwenye Kanisa la KKKT  Usharika wa Ilongelo kwa ajili ya ibada maalum. Pamona nao ni watoto wao Sera na Christopher kabla ya kwenda Uwanjani kutangaza azma yake ya kuwania Urais 2015.
Nyalandu na Faraja Kota wakiwa na watoto wao Sera na Christopher katika kanisa hilo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro  Nyalandu akitoa neno la shukrani baada ya ibada maalum katika katisa la KKKT Usharika wa Ilongelo jimboni humo.
Waziri Nyalandu akiwa na watoto wake wakati wa ibada maalum iliyofanyilka katika Kanisa la KKKT Usharika wa Ilongelo Jimbo la Singida Kaskazini.
Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu akitoa sadaka wakati wa ibada maalum iliyofanyika  katika Kanisa la KKKT Usharika wa Ilongelo jimboni humo.
Mke wa NYalandu, Faraja Kota akipita baada ya kutoa sadaka kwenye kanisa hilo la KKKT Usharika wa Ilongelo.
Mwimbaji wa nyimbo za Injili lkatika Kanisa la KKKT Usharika wa Ilongelo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu akizungumza na viongozi wa shule ya Kiislam ambayo huhudumia watoto wa dini zote katika kata ya Ilongelo, shule hiyo ina watoto 74.
Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu akisalimia waumini kwenye Kanisa la FPCT  katika jimbo la Ilongelo alipofika kwa ajili ya ibada maalum.
Waumini wakiwa katika kanisa la FPCT wakati wa ibada maalum aliyohudhuria Nyalandu.
Nyalandu na Mkewe wakitoka katika Kanisa la FPCT baada ya kuhudhuria ibada maalum asubuhi.
Mbunge wa Singida Kaskazini, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu ametangaza rasmi kuwania Urais wa Tanzania katika uchaguzi mkuu mwakani.
Amesema amechukua uamuzi huo baada ya kuona kwamba anao uwezo wa kuiongoza Tanzania, katika harakati za kuwafikisha kwenye maendeleo endelevu wanayotaka Watanzania.
Amesema, yuko tayari kushindanishwa na Watanzania wengine watakaoona kuwa wanafaa kuwa Rais, lakini akisema kwanza kila atakayejitokeza itabidi kazi zake zipimwe kwa moto na endapo zitayeyuka hafai.
Nyalandu ambaye alitangaza uamuzi huo kwenye Uwanja wa Michezo wa Ilongelo jimbo la Singida Kaskazini, alisema, yeye anaingia kwenye kinyang'anyiro akiwa kifua mbele kutokana na kuamini kwamba amekwishafanyakazi zilizotukuka.
"Kazi zangu nilizofanya zinajulikana na ninaziamini kwamba ni nzuri, hivyo yeyote atakayetaka urais apimanishwe na mimi kwa kupimwa kazi zetu kwa moto", alisema Nyalandu
Itakapofika siku ya siku, nitaenda Dodoma nikisindikizwa na wana Singida Mashariki, na wengine wengi kutoka pembe zote za Tanzania, kwenda Dodoma kuchukua fomu ya kuwania kuteuliwa kugombea Urais kwa tiketi ya CCM", alisema.
Mkutano huo wa jimbo ambao ulipambwa na shamrashamra mbalimbali zikiwemo za wasanii wakiwemo kina Rose Mhando, ulifurika maelfu ya wananchi waliohamasika kumsikiliza Nyalandu.
+

Wednesday 17 December 2014

Catherine Samba-Panza: ‘Kigogo’ aliyemaliza maafa Afrika ya Kati


 
.


Watu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati na Jumuiya ya Kimataifa haitasahau namna mwama mama Catherine Samba alivyorejesha amani na mshikamano katika nchi hiyo.
Catherine aliyekuwa Meya wa Jiji la Bangui kuanzia Mei mwaka 2013, alipata nafasi ya pekee ya kupendekezwa kushika wadhifa wa urais wa mpito miezi minane baadaye na kisha kuapishwa Januari 23, 2014 siku 12 tangu kuachia ngazi wa Dtojidia.
Catherine aliyezaliwa Juni 26, 1954 alivunja rekodi na kuweka historia kwa kuwa rais wa kwanza wa mpito kwa miezi 18 ambayo bado anaitumikia, lakini pia kuwa rais wa kwanza mwanamke katika taifa hilo lililokuwa likipitia kipindi cha mpito kutokana na machafuko makali.
Aliteuliwa kuwa Meya wa Jiji la Bangui, mji Mkuu wa CAR chini ya Baraza la Mpito la Taifa (CNT) baada ya mgogoro uliolikabili taifa hilo kwa karibu mwaka mmoja, kuanzia mwaka 2012.
Uteuzi wake ulikubaliwa na pande zote mbili ziliziokuwa zikipingana, upande wa Seleka na Anti-balaca.
Katika uteuzi huo, Catherine ambaye alikuwa mwanasheria na mfanyabiashara kabla ya kuingia katika siasa alikubalika pia na Rais Francois Hollande wa Ufaransa, ambaye alikuwa akitafuta namna ya kumaliza mgogoro wa taifa hilo.
Hata hivyo, awali hakutarajiwa kupata nafasi hiyo ya kuwa rais wa mpito, kwa kuwa kulikuwa na zaidi ya watu wanane waliokuwa wakitajwa kufikiriwa kupewa nafasi hiyo, lakini walitakiwa kuthibitisha kwamba hawana uhusiano na makundi hayo mawili, yaani Seleka na Anti-balaka.
Suala la kwanza, mama huyo anaweka historia na kuwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo na zaidi kwa kufanikiwa kurejesha amani na utulivu kuelekea kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani.
Hotuba yake aliyoitoa kwa ujasiri baada ya kuthibitishwa na bunge la nchi hiyo akiwataka wahusika kuweka chini zana zao na kusitisha mapigano ilikuwa na matunda makubwa.
Hakusita kuugeukia upande wa pili wa Seleca ambao kwa kuwa walikuwa ndio waathirika wakubwa, aliwataka waache woga na kwamba hakuwa tayari kusikia tena mauaji ya watu wasio na hatia, kwa kujipambanua kwamba ni rais wa watu wote bila kuwa na ubaguzi.
Wito wake wa kutaka mazungumzo baina ya pande mbili zilizohusika kwenye mgogoro wa kisiasa uliitikiwa kikamilifu na pande zote mbili, na japokuwa aliingia madarakani katika kipindi ambacho hakikuwa na utawala wa sheria, aliweza kurejesha taifa hilo kwenye mstari na kuepuka kile kilichohofiwa kutokea, mauaji makubwa ya kimbari kama ilivyowahi kutokea Rwanda.
Chanzo cha machafuko
Machafuko katika nchi hiyo yalishika kasi baada ya Rais Michael Dtojodia kupindua Serikali na kuchukua madaraka.
Hatua hiyo ilivuruga amani ya taifa hilo na kuibua mapambano baina ya makundi mawili yaliyokuwa na mitizamo ya kidini, Seleka na Anti-Balaka kuingia katika machafuko yaliyolielekeza taifa hilo kwenye vita ya wenyewe kwa wenyewe.
Baada ya Djotodia aliyeingia madarakani Machi 24, 2013 kwa kumuondoa Rais Francois Bozize, kukubali kuachia madaraka Januari 10 mwaka huu kutokana na shinikizo kali la ndani na Jumuiya ya Kimataifa, alitoa nafasi ya kuibuka kwa mwanamama Catherine.
+

SPIKA MARGARET ZZIWA ASIMAMISHWA


HATIMAYE Spika wa Bunge la Afrika Mashariki, Dk. Margaret Zziwa (pichani) amesimamishwa wadhifa huo baada ya wabunge wa bunge hilo kumpigia kura. Apewa saa 24 kukabidhi ofisi ya bunge.
+

Saturday 13 December 2014

Watuhumiwa Escrow wajiengue: Maria Nyerere


Mama Maria akikabidhiwa tunzo ya amani
Mama Maria Nyerere, (pichani)  amesema waliotuhumiwa kula fedha za akaunti ya Escrow walipaswa kujiengua katika nafasi zao badala ya kumsubiri Rais atoe maamuzi.
“Hivi karibuni tumeshuhudia mambo yaliyotokea bungeni, wananchi wameona, nilitegemea waliotajwa wangejiondoa wenyewe katika nafasi zao badala ya kusubiria Rais,” alisema.
Mama Maria alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam, mara baada ya kukabidhiwa tunzo ya amani iliyotolewa na Kamati ya mkesha mkubwa kitaifa na dua maalum inayotarajia kufanyika nchini Desemba 31, mwaka huu.
Kauli hiyo ya Mama Maria, inafuatia mjadala mkubwa ulioibuka bungeni hivi karibuni mjini Dodoma baada ya Wabunge kumtaka Waziri wa Nishati na Madini. Profesa Sospeter Muhongo, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Eliakim Maswi, Waziri wa Ardhi, Nyuma na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, kutakiwa kujiuzulu baada ya kutuhumiwa kuhusika na sakata hilo.
Katika sakata hilo, imedaiwa kuibwa kiasi cha Sh. bilioni 306 zilizochotwa kwenye akaunti hiyo na kuhusisha watu mbalimbali wakiwamo wafanyabishara na baadhi ya viongozi wa serikali.
Aidha, Mama Maria  alisema nchi inahitaji maombi ya pamoja ili kunusuru taifa kuingia katika machafuko, kutokana na yanayojitokeza hivi sasa.
Mara baada ya kukabidhiwa tunzo hiyo alisema viongozi wa mwanzo walipewa unyenyekevu na kuweza kupita katika mawimbi na dhoruba.
“Makosa mengine yametokana na uzembe na utu hivyo tunahitaji maombi ya pamoja mimi naiombea sana nchi yangu, hali tuliyonayo amani kidogo Mungu anatukumbusha tumkumbuke, tuwe watu wa sala na kazi,” alisema.
Kuhusu vitendo vya ukatili vya kuwaua na kuwajeruhi watu wenye ulemavu wa ngozi, alisema ni vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vinapaswa kukomeshwa.
Aliwataka Watanzania kuhakikisha maombi yao wanayaelekeza kwenye nchi nyingine ili kuwakomboa na matatizo yanayowakabili ya magonjwa na vita.
 “Tulio wengi katika nchi hii ni watu wenye upendo ni kama tumependelewa, ndiyo maana nasema viongozi wetu wa awali walipewa unyenyekevu,” alisema. Alitolea mfano wa baadhi ya mambo yaliyotokea awali kuwa ni vita vya Kagera ambayo alisema haikuwa kitu kidogo lakini viongozi waliongozwa kupita kwenye hilo na kuyamaliza. Alisema kwa sasa yapo magonjwa kama ebola, mabadiliko ya tabia nchi na mambo mengine ambayo yanahitaji maombi.
Mjumbe wa kamati iliyomkabidhi tunzo hiyo, Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Pentekoste, William Mwamalanga, alisema tunzo waliyompa ni ya  kuhamasisha amani Tanzania.
Alisema tunzo kama hizo wametoa kwa watu mbalimbali na kuwataja baadhi kuwa ni Rais Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba na Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi.
+

Saturday 6 December 2014

KIFIMBO CHA MWALIMU NYERERE KILIKUWA NA NGUVU FULANI?

Hayati Mwalimu Nyerere enzi za uhai wake. KWA miaka mingi watu wamekuwa wakitoa maelezo kadha wa kadhaa kuhusu kifimbo ambacho Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikibeba kila alipokwenda.
Kuna ambao walisema hakikuwa  kifimbo cha kawaida na kuna waliokihusisha kifimbo hicho na zindiko.
Kuna ambao bado wanasema kifimbo cha Nyerere kilikuwa na nguvu fulani ya asili na ya kimila ambayo ilimfanya aheshimike na kuogopwa.
Mwandishi wa vitabu, W.E. Smith, katika kitabu chake kuhusu maisha ya Mwalimu Nyerere, ananukuliwa akizungumzia nguvu za jadi kwenye kabila lake (Nyerere) la Wazanaki.
Katika kitabu hicho Smith ananukuu baadhi ya maoni ya Mwalimu kuhusu nguvu za jadi, hasa katika jamii za Kiafrika.
Anaeleza kuwa Mwalimu, Aprili 1966, aliulizwa kama angeweza kueleza katika lugha ya Kiingereza kuhusu manyoya ya mbuzi ambayo yalichanganywa na nywele zake, ili kusababisha mbuzi aliopewa na ndugu zake aswagwe kwa urahisi hadi nyumbani kwao.
Smith anamnukuu Mwalimu Nyerere akisema: “Nilipokuwa na umri wa kiasi cha miaka 10, siku mmoja baba (Chifu Nyerere Burito) alinituma nifuatane na mke wake wa kwanza, mmoja wa mama zangu wa kambo, kwenda katika kijiji kingine, umbali wa maili nane au kumi hivi, ambako mmoja wa jamaa zake huyo mama, alikuwa amefariki.
“Tulipokaribia kuondoka katika kijiji hicho, kurudi nyumbani, ndugu zake wakampa mbuzi. Lakini mbuzi yule alikataa kutii kuondoka. Na wakati nilipokuwa nakurupushana naye, mmoja wa jamaa za mama yangu wa kambo akasema, ‘usiwe na wasiwasi. Nitakurahisishia kazi.’
“Basi, akang’oa nywele kidogo kutoka kichwani kwangu na manyoya kidogo kutoka katika kichwa cha yule mbuzi. Akazichanganya na mizizi fulani, akatafunia pamoja na halafu akampa mbuzi, akala.
“Akasema ‘sasa mbuzi atakufuata.’ Na kweli mbuzi akanifuata njia yote mpaka nyumbani. Ndiyo, alikuwa ameelekea kabisa. Alinifuata kama mbwa,” anasema Mwalimu katika kitabu cha Smith.
Smith anamnukuu Mwalimu akisema, “Mimi sidhani ni vigumu kama watu wanavyofikiri. Katika maisha ya kikabila, kijana anapofikia umri wa miaka 12 huwa karibu amehitimu. Ndiyo, unajua mambo mengi ya maisha katika umri wa miaka 12 mtu hufundishwa.
“Unayajua yote unayotakiwa uyajue, ambayo hujulikana hadharani. Lakini lazima unafichwa sana siri za wazee.”
Mwandishi anamnukuu Mwalimu enzi hizo akisema kuwa Wakristo wanayakataa mawazo ya kikabila, huku wakiwa na sababu chache za kufanya hivyo, kwa sababu hata wenyewe wanaamini vitu ambavyo haviwezi kuelezeka.
“Ninalofahamu mimi ni kwamba yule mbuzi alinifuata. Na nikijitahidi sana kufikiri naweza tu kusema, sijui,” anaeleza Mwalimu.
Masimulizi kuhusu mbuzi ndiyo yamefanya wengi kuamini kuwa kifimbo cha Mwalimu kinaweza kuwa na nguvu za asili kama nguvu za kufanya mbuzi afuate mtoto kama mbwa, badala ya kuswagwa.
Aidha, ile tabia yake ya kuwa na kifimbo chake popote alipokwenda, iliongeza tetesi na kukuza mjadala. Je, kulikuwa na nguvu yoyote ya kijadi ndani yake?
Bali kuna taarifa kuwa Mwalimu hakuwa na kifimbo kimoja. Makumbusho yake yaliyopo Butiama, Musoma Vijijini, yanaonyesha kuwa vipo vifimbo vyake vingi na mkwaju aliotumia wakati wa kupigania uhuru.
Bado kitendawili hakijateguliwa na bado wanahistoria wana kazi kubwa ya kufanya utafiti wa kifimbo cha Nyerere.
+

Friday 5 December 2014

Zitto: Nina sharti moja tu kurudi Chadema


 


Dar es Salaam. Harufu ya kuisha kwa mgogoro baina ya Zitto Kabwe na chama chake cha Chadema inanukia, lakini mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini anataka kuwapo na mazungumzo kubaini tatizo ili atakayebainika kuwa alifanya makosa awe tayari kuomba radhi hadharani.
Zitto alikiri bungeni kuwa amekuwa “akimiss” harakati zilizokuwa zikifanywa na vyama vya upinzani wakati wa Bunge Maalumu la Katiba, harakati zilizozaa Umoja wa Katiba ya Wananchi na kufurahia kuhudhuria kwa mara ya kwanza vikao vya umoja huo.
Zitto, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), alipata fursa ya kuingia vikao vya Ukawa wakati wapinzani walipoungana tena kupambana dhidi ya wizi wa fedha kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow, sakata ambalo liliwekwa bayana na kamati yake baada ya Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila kulifikisha bungeni, lakini hakudokeza lolote kuhusu Chadema.
Hata hivyo, mapema wiki hii, Zitto, ambaye Novemba mwaka jana alivuliwa nyadhifa zote kwenye chama hicho kwa tuhuma za kukihujumu, lakini akafanikiwa kulinda uanachama wake baada ya kufungua kesi mahakamani na kufanikiwa kupata amri ya kuzuia asijadiliwe.
Baada ya kuongoza PAC kuchunguza wa tuhuma za Escrow na kufanikiwa kulishawishi Bunge kufikia maazimio manane ya kuwashughulikia kisheria wahusika kwenye uchotwaji huo wa fedha, kumekuwapo na wito kutoka kwa baadhi ya wafuasi wa Chadema kutaka pande hizo mbili zimalizane.
“Kabla ya jambo lolote kufanyika, ili kukata kiu ya Watanzania wanaotaka kuona tunaondoa tofauti zetu, ni lazima kusema ukweli na kila upande kuwa tayari kuomba radhi hadharani pindi ikibainika ulifanya makosa,” alisema Zitto alipotakiwa kuzungumzia harakati hizo za kumrejesha Chadema.
“Ukweli wangu ndani ya Chadema ni nini? Lakini mimi ninaona sina kosa ndani ya Chadema. Ninachotaka mimi nielezwe ukweli bila chembe ya shaka makosa yangu mimi ni nini,” alisema na kuongeza:
“Nitakuwa tayari kuomba radhi hadharani kama ikibainika nilifanya makosa na kama ikibainika chama kilifanya makosa, nacho kiwe tayari kuomba radhi hadharani na ukweli uwe mbele katika maridhiano.
“Kama hakutakuwa na ukweli itakuwa vigumu kupata mwafaka. Mimi sina tatizo. Nirudie nilivyosema bungeni kuwa nina-miss sana (ninapenda sana kuwamo kwenye) harakati za mageuzi kipindi hiki za kuiondoa CCM madarakani.”
Katika mkutano na waandishi wa habari mara baada ya kuvuliwa nyadhifa zote, Zitto alisema: “Natambua kuwa wapo ambao wangependa kutumia nafasi zao kudhoofisha mapambano ya siasa za demokrasia nchini mwetu. Napenda wanachama wa Chadema na wapenda demokrasia watambue kuwa, mimi bado ni mwanachama mwaminifu wa chama hiki.
“Kinachoendelea ndani ya chama chetu ni mapambano ya kukuza demokrasia. Ni mapambano baina ya wapenda demokrasia dhidi ya wahafidhina; waumini wa uwajibikaji dhidi ya wabadhirifu; na wapenda siasa safi dhidi ya watukuzao siasa majitaka.”
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, ambaye binafsi aliguswa na mzozo huo, hakuwa tayari kuzungumzia kumaliza matatizo baina ya chama na Zitto.
“No comment (sina maoni) kwa hilo. Siwezi kuzungumzia suala hili katika media (vyombo vya habari),” alisema Mbowe
Hoja ya kutaka Zitto arejeshwe Chadema imekuwa ikisambaa katika mitandao ya kijamii na kwa baadhi ya wanasiasa baada ya kuonekana kuwa karibu na viongozi wa chama chake wakati Kamati ya PAC ilipoibua ufisadi wa Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow wiki iliyopita.
Wakati akihitimisha mjadala wa sakata la Escrow, mbali na kueleza bayana kuwa alifurahia kuhudhuria vikao vya Ukawa kwa mara ya kwanza, Zitto alikwenda mbali na kumpongeza “kwa namna ya pekee” Mbowe kwa jinsi walivyoshirikiana katika sakata hilo.
Zitto alisema hilo lilikuwa ni jambo la kitaifa ndiyo maana wabunge wote wa upinzani bila kujali vyama vyao waliungana.
Alisema mara baada ya sakata hilo kumalizika watu mbalimbali wamekuwa wakizungumzia kufanyika kwa maridhiano ili awe sehemu ya Ukawa na kwamba haoni tatizo.
“Katika hili, kipekee namshukuru kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani kwa kuniunga mkono katika sakata hili,” alisema Zitto.
Kuhusu taarifa za kujiunga kwake na chama kipya cha ACT-Tanzania alisema: “Hizo ni taarifa ambazo hazina ukweli wowote.”
Kuhusu kesi aliyofungua mahakamani dhidi ya Chadema, Zitto alisema:
“Nilifungua kesi kwa sababu ya kulinda uanachama wangu, lakini mazungumzo yakifanyika na kujua kosa langu ni nini, nitaifuta kesi hiyo na kuanza upya harakati.”
Zitto.
Kuhusu taarifa za kujiunga kwake na chama kipya cha ACT-Tanzania alisema, “Hizo ni taarifa ambazo hazina ukweli wowote.”
Kuhusu kesi aliyofungua mahakamani dhidi ya Chadema, Zitto alisema: “Nilifungua kesi kwa sababu ya kulinda uanachama wangu, lakini mazungumzo yakifanyika na kujua kosa langu ni nini, nitaifuta kesi hiyo na kuanza harakati.”
+