Saturday 13 December 2014

Leave a Comment

Watuhumiwa Escrow wajiengue: Maria Nyerere


Mama Maria akikabidhiwa tunzo ya amani
Mama Maria Nyerere, (pichani)  amesema waliotuhumiwa kula fedha za akaunti ya Escrow walipaswa kujiengua katika nafasi zao badala ya kumsubiri Rais atoe maamuzi.
“Hivi karibuni tumeshuhudia mambo yaliyotokea bungeni, wananchi wameona, nilitegemea waliotajwa wangejiondoa wenyewe katika nafasi zao badala ya kusubiria Rais,” alisema.
Mama Maria alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam, mara baada ya kukabidhiwa tunzo ya amani iliyotolewa na Kamati ya mkesha mkubwa kitaifa na dua maalum inayotarajia kufanyika nchini Desemba 31, mwaka huu.
Kauli hiyo ya Mama Maria, inafuatia mjadala mkubwa ulioibuka bungeni hivi karibuni mjini Dodoma baada ya Wabunge kumtaka Waziri wa Nishati na Madini. Profesa Sospeter Muhongo, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Eliakim Maswi, Waziri wa Ardhi, Nyuma na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, kutakiwa kujiuzulu baada ya kutuhumiwa kuhusika na sakata hilo.
Katika sakata hilo, imedaiwa kuibwa kiasi cha Sh. bilioni 306 zilizochotwa kwenye akaunti hiyo na kuhusisha watu mbalimbali wakiwamo wafanyabishara na baadhi ya viongozi wa serikali.
Aidha, Mama Maria  alisema nchi inahitaji maombi ya pamoja ili kunusuru taifa kuingia katika machafuko, kutokana na yanayojitokeza hivi sasa.
Mara baada ya kukabidhiwa tunzo hiyo alisema viongozi wa mwanzo walipewa unyenyekevu na kuweza kupita katika mawimbi na dhoruba.
“Makosa mengine yametokana na uzembe na utu hivyo tunahitaji maombi ya pamoja mimi naiombea sana nchi yangu, hali tuliyonayo amani kidogo Mungu anatukumbusha tumkumbuke, tuwe watu wa sala na kazi,” alisema.
Kuhusu vitendo vya ukatili vya kuwaua na kuwajeruhi watu wenye ulemavu wa ngozi, alisema ni vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vinapaswa kukomeshwa.
Aliwataka Watanzania kuhakikisha maombi yao wanayaelekeza kwenye nchi nyingine ili kuwakomboa na matatizo yanayowakabili ya magonjwa na vita.
 “Tulio wengi katika nchi hii ni watu wenye upendo ni kama tumependelewa, ndiyo maana nasema viongozi wetu wa awali walipewa unyenyekevu,” alisema. Alitolea mfano wa baadhi ya mambo yaliyotokea awali kuwa ni vita vya Kagera ambayo alisema haikuwa kitu kidogo lakini viongozi waliongozwa kupita kwenye hilo na kuyamaliza. Alisema kwa sasa yapo magonjwa kama ebola, mabadiliko ya tabia nchi na mambo mengine ambayo yanahitaji maombi.
Mjumbe wa kamati iliyomkabidhi tunzo hiyo, Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Pentekoste, William Mwamalanga, alisema tunzo waliyompa ni ya  kuhamasisha amani Tanzania.
Alisema tunzo kama hizo wametoa kwa watu mbalimbali na kuwataja baadhi kuwa ni Rais Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba na Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi.

0 comments: