Wednesday 17 December 2014

Leave a Comment

Maximo anatia huruma, awaaga wachezaji kwa majonzi

Kocha Mkuu wa Yanga, Mbrazili, Marcio Maximo. Na Waandishi Wetu
AKIWA na uso wa huzuni, aliyekuwa Kocha Mkuu wa Yanga, Mbrazili, Marcio Maximo, jana alifika kwenye mazoezi ya timu hiyo asubuhi na kuwaaga wachezaji wake.
Hiyo ni baada ya kupewa taarifa za kutimuliwa na uongozi wa timu hiyo kufuatia kipigo cha mabao 2-0 walichokipata dhidi ya Simba katika mechi ya Nani Mtani Jembe iliyochezwa wikiendi iliyopita.
Maximo alifika mazoezini hapo saa 2:35 akiwa na msaidizi wake, Leonardo Neiva, kiungo mkabaji wa timu hiyo raia wa Brazili, Emerson De Oliviera, ambao wote wamesitishiwa mikataba yao kwa ajili ya kuwaaga na Andrey Coutinho ambaye aliachwa kuendelea na mazoezi huku hao wengine wakiondoka.
Mbrazili huyo, aliwaaga wachezaji hao, zoezi lililotumia dakika kumi kwenye Uwanja wa Loyola, Mabibo jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka na gari ndogo aina ya Toyota Hiace kuelekea hotelini alipokwenda kufanya mazungumzo na viongozi wa timu hiyo.
Kwa mujibu wa mmoja wa wachezaji wa timu hiyo, kocha huyo mara baada ya kufika uwanjani hapo, aliwaita wachezaji hao na kuzungumza nao mambo mbalimbali kuhusiana na timu.Chanzo hicho kilisema, katika mazungumzo yake aliwatakia kila la kheri wachezaji na viongozi aliowaacha, Shadrack Nsajigwa na Salvatory Edward katika kuipa mafanikio ya mataji ya ubingwa kwa kuanzia na Ligi Kuu Bara.
“Inasikitisha kiukweli kocha wetu kufukuzwa ghafla, wamemshtukiza, ilitakiwa wampe muda kidogo wa kuiandaa timu na siyo kumfukuza baada ya kufungwa na Simba katika Nani Mtani Jembe.
“Alifika leo asubuhi akiwa na msaidizi wake, Neiva, Emerson na Coutinho kwa ajili ya kutuaga wachezaji, baada ya kufika tukazungumza naye kama dakika kumi na baadaye akaingia kwenye gari na kuondoka na kumuacha Coutinho akiendelea na mazoezi.
“Aliongea maneno mengi, lakini kikubwa alitutia moyo wa kuendelea kufanya vizuri katika mechi za ligi kuu na kututaka kumpa ushirikiano kocha mpya atakayekuja kutufundisha,” alisema mchezaji huyo huku akionekana kuwa na majonzi.
Maximo ambaye ameiacha Yanga ikiwa katika nafasi ya pili kwenye ligi akiwa kwenye gari wakati anatoka kwenye lango la Loyola, alionekana kuwa na huzuni kubwa, huku akikuna kichwa.

0 comments: